Text copied!
Bibles in Swahili (individual language)

Matendo 4:7-28 in Swahili (individual language)

Help us?

Matendo 4:7-28 in Biblia Takatifu

7 Waliwasimamisha mitume mbele yao, wakawauliza, “Ninyi mmefanya jambo hili kwa nguvu gani na kwa jina la nani?”
8 Hapo, Petro, akiwa amejawa na Roho Mtakatifu, akawaambia, “Viongozi na wazee wa watu!
9 Ikiwa mnatuuliza leo juu ya kile kitendo chema alichofanyiwa yule mtu aliyekuwa kiwete na jinsi alivyopata kuwa mzima,
10 basi, ninyi na watu wote wa Israeli mnapaswa kujua kwamba mtu huyu anasimama mbele yenu leo, mzima kabisa, kwa nguvu ya jina lake Yesu wa Nazareti ambaye ninyi mlimsulubisha, lakini Mungu akamfufua kutoka wafu.
11 Huyu ndiye ambaye Maandiko Matakatifu yanasema: Jiwe mlilokataa ninyi waashi, sasa limekuwa jiwe kuu la msingi.
12 Wokovu haupatikani kwa mtu mwingine yeyote, kwa maana duniani pote, binadamu hawakupewa jina la mtu mwingine ambaye sisi tunaweza kuokolewa naye.”
13 Hao wazee wa baraza, wakiwa wanajua kwamba Petro na Yohane walikuwa watu wasio na kisomo wala elimu yoyote, walishangaa juu ya jinsi walivyosema kwa uhodari. Wakatambua kwamba walikuwa wamejiunga na Yesu.
14 Lakini walipomwona yule mtu aliyeponywa amesimama pamoja nao, hawakuweza kusema kitu.
15 Hivyo, waliwaamuru watoke nje ya baraza, nao wakabaki ndani wakizungumza kwa faragha.
16 Wakaulizana, “Tufanye nini na watu hawa? Kila mtu anayeishi Yerusalemu anajua kwamba mwujiza huu wa ajabu umefanyika, nasi hatuwezi kukana jambo hilo.
17 Lakini ili tupate kuzuia jambo hili lisienee zaidi kati ya watu, tuwaonye wasiongee na mtu yeyote kwa jina la Yesu.”
18 Kwa hiyo wakawaita tena ndani, wakawaonya wasiongee tena hadharani, wala kufundisha kwa jina la Yesu.
19 Lakini Petro na Yohane wakawajibu, “Amueni ninyi wenyewe kama ni haki mbele ya Mungu kuwatii ninyi kuliko kumtii yeye.
20 Kwa maana hatuwezi kuacha kusema juu ya mambo yale tuliyoyaona na kuyasikia.”
21 Basi, hao wazee wa Baraza wakawaonya kwa ukali zaidi, halafu wakawaacha huru. Hawakuweza kuwapa adhabu kwa sababu watu wote walikuwa wakimtukuza Mungu kwa sababu ya tukio hilo.
22 Huyo mtu aliyeponywa alikuwa na umri wa miaka zaidi ya arobaini.
23 Mara tu walipoachwa huru, Petro na Yohane walirudi kwa wenzao, wakawaeleza yale waliyoambiwa na makuhani wakuu na wazee.
24 Waliposikia habari hiyo waliungana pamoja katika kumwomba Mungu wakisema, “Bwana, wewe ni Muumba wa mbingu na nchi, bahari na vyote vilivyomo!
25 Ndiwe uliyemfanya mtumishi wako, babu yetu Daudi, aseme kwa nguvu ya Roho Mtakatifu: Kwa nini mataifa yameghadhibika? Mbona watu wamefanya mipango ya bure?
26 Wafalme wa dunia walijiweka tayari, na watawala walikutana pamoja, ili kumwasi Bwana na Kristo wake.
27 “Maana, kwa hakika, ndivyo Herode, Pontio Pilato, watu wa Israeli na watu wa mataifa walivyokutanika papa hapa mjini, kumpinga Yesu Mtumishi wako Mtakatifu ambaye umemtia mafuta.
28 Naam, walikutana ili wafanye yale ambayo ulikusudia na kupanga tangu mwanzo kwa uwezo wako na mapenzi yako.
Matendo 4 in Biblia Takatifu

Matendo ya Mitume 4:7-28 in Biblia ya Kiswahili

7 Walipokuwa wamewaweka Petro na Yohana katikati yao, waliwauliza, “Kwa uwezo gani, au kwa jina gani mmefanya hili?”
8 Kisha, Petro, akiwa amejaa Roho Mtakatifu, akawaambia, “Ninyi wakuu wa watu, na wazee,
9 kama sisi siku ya leo tunahojiwa kuhusu tendo jema lililofanywa kwa mtu huyu mgonjwa - kwa namna gani mtu huyu alifanywa mzima?
10 Hebu lijulikane hilo kwenu na kwa watu wote katika Israel, kwamba kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, ambaye mlimsulibisha, ambaye Mungu alimfufua kutoka kwa wafu, ni kwa njia yake kwamba mtu huyu anasimama hapa mbele yenu akiwa mwenye afya.
11 Yesu Kristo ni jiwe ambalo ninyi wajenzi mlilidharau, lakini ambalo limefanywa kuwa jiwe kuu la pembeni.
12 Hakuna wokovu katika mtu mwingine awaye yote. Kwa maana hakuna jina jingine chini ya mbingu walilopewa watu, ambalo kwa hilo tunaweza kuokolewa.”
13 Sasa walipoona ujasiri wa Petro na Yohana, na wakagundua kwamba walikuwa ni watu wakawaida wasio na elimu, walishangaa, wakafahamu kwamba Petro na Yohana wamekuwa pamoja na Yesu.
14 Kwa sababu walimwona yule mtu aliyeponywa amesimama pamoja nao, hawakuwa na kitu cha kusema dhidi ya hili.
15 Lakini walipokuwa wamekwisha kuwaamuru mitume waondoke mbele ya mkutano wa baraza, walizungumza wao kwa wao.
16 Walisema, tutawafanyaje watu hawa? Ni kweli kwamba muujiza wa ajabu umefanyika kupitia wao unajulikana na kila mmoja anayeishi Yerusalemu; hatuwezi kulikataa hilo.
17 Lakini, ili kwamba jambo hili lisienee miongoni mwa watu, hebu tuwaonye wasinene tena kwa mtu yeyote kwa jina hili.
18 Waliwaita Petro na Yohana ndani na kuwaamuru kamwe wasinene wala kufundisha kwa jina la Yesu.
19 Lakini Petro na Yohana walijibu na kuwaambia, “Kama ni sahihi machoni pa Mungu kuwatii ninyi kuliko Mungu, hukumuni wenyewe.
20 Maana sisi hatuwezi kuacha kuyanena mambo ambayo tumeyaona na kuyasikia.”
21 Baada ya kuwaonya sana Petro na Yohana, waliwaacha waende. Hawakuweza kupata sababu yoyote ya kuwaadhibu, kwa sababu watu wote walikuwa wakimsifu Mungu kwa kile kilichokuwa kimetendeka.
22 Mtu aliyekuwa amepokea muujiza wa uponyaji alipata kuwa na umri zaidi ya miaka arobaini.
23 Baada ya kuwaacha huru, Petro na Yohana walikuja kwa watu wao na kuwataarifu yote ambayo makuhani wakuu na wazee walikuwa wamewaambia.
24 Walipoyasikia, walipaza sauti zao kwa pamoja kwa Mungu na kusema, “Bwana, wewe uliyeumba mbingu na dunia na bahari na kila kitu ndani yake,
25 wewe ambaye, kwa Roho Mtakatifu, kwa kinywa cha baba yetu Daudi, mtumishi wako, ulisema, “Kwanini watu wa mataifa wamefanya ghasia, na watu wametafakari mambo yasiyofaa?
26 Wafalme wa dunia wamejipanga pamoja, na watawala wamekusanyika kwa pamoja dhidi ya Bwana na dhidi ya masihi wake.”
27 Ni hakika, wote Herode na Pontio Pilato, pamoja na watu wa mataifa na watu wa Israeli, walikusanyika kwa pamoja katika mji huu dhidi ya mtumishi wako mtakatifu Yesu, ambaye ulimpaka mafuta.
28 Walikusanyika kwa pamoja kufanya yote ambayo mkono wako na mapenzi yako yaliyaamuru tangu awali kabla hayajatokea.
Matendo ya Mitume 4 in Biblia ya Kiswahili