Text copied!
Bibles in Swahili (individual language)

Marko 6:9-53 in Swahili (individual language)

Help us?

Marko 6:9-53 in Biblia Takatifu

9 Vaeni viatu lakini msivae kanzu mbili.”
10 Tena aliwaambia, “Popote mtakapokaribishwa nyumbani, kaeni humo mpaka mtakapoondoka mahali hapo.
11 Mahali popote ambapo watu watakataa kuwakaribisheni au kuwasikiliza, ondokeni hapo na kuyakung'uta mavumbi miguuni mwenu kama onyo kwao.”
12 Basi, wakaondoka, wakahubiri watu watubu.
13 Waliwafukuza pepo wengi wabaya; wakawapaka mafuta wagonjwa wengi, wakawaponya.
14 Basi, mfalme Herode alisikia juu ya hayo yote, maana sifa za Yesu zilienea kila mahali. Baadhi ya watu walikuwa wakisema, “Yohane Mbatizaji amefufuka kutoka wafu, ndiyo maana nguvu za miujiza zinafanya kazi ndani yake.”
15 Wengine walisema, “Mtu huyu ni Eliya.” Wengine walisema, “Huyu ni nabii kama mmojawapo wa manabii wa kale.”
16 Lakini Herode alipopata habari hizi alisema, “Huyu ni Yohane! Nilimkata kichwa, lakini amefufuka.”
17 Hapo awali Herode mwenyewe alikuwa ameamuru Yohane atiwe nguvuni, akamfunga gerezani. Herode alifanya hivyo kwa sababu ya Herodia ambaye Herode alimwoa ingawaje alikuwa mke wa Filipo, ndugu yake.
18 Yohane alikuwa amemwambia Herode, “Si halali kwako kumchukua mke wa ndugu yako.”
19 Basi Herodia alimchukia sana Yohane, akataka kumwua, asiweze.
20 Herode alimwogopa Yohane kwa maana alijua kwamba yeye ni mtu mwema na mtakatifu, na hivyo akamlinda. Herode alipenda kumsikiliza Yohane, ingawaje baada ya kumsikiliza, alifadhaika sana.
21 Ikapatikana nafasi, wakati wa sikukuu ya kuzaliwa kwake Herode. Herode aliwafanyia karamu wazee wa baraza lake, majemadari na viongozi wa Galilaya.
22 Basi, binti yake Herodia aliingia, akacheza, akawafurahisha sana Herode na wageni wake. Mfalme akamwambia huyo msichana, “Niombe chochote utakacho, nami nitakupa.”
23 Tena akamwapia, “Chochote utakachoniomba, nitakupa: hata ikiwa ni nusu ya ufalme wangu.”
24 Hapo huyo msichana akatoka, akamwuliza mama yake, “Niombe nini?” Naye akamjibu, “Kichwa cha Yohane mbatizaji.”
25 Msichana akamrudia mfalme mbio akamwomba, “Nataka unipe sasa hivi katika sinia kichwa cha Yohane mbatizaji.”
26 Mfalme akahuzunika sana, lakini kwa sababu ya kiapo chake, na kwa ajili ya wale wageni wake karamuni, hakutaka kumkatalia.
27 Basi, mfalme akamwamuru askari kukileta kichwa cha Yohane. Askari akaenda, akamkata kichwa Yohane mle gerezani,
28 akakileta katika sinia, akampa msichana naye msichana akampa mama yake.
29 Wanafunzi wa Yohane walipopata habari, walikwenda wakachukua mwili wake, wakauzika kaburini.
30 Wale mitume walirudi, wakakusanyika mbele ya Yesu wakamwarifu yote waliyotenda na kufundisha.
31 Alisema hivyo kwa kuwa kulikuwa na watu wengi mno walikuwa wanafika hapo na kuondoka hata Yesu na wanafunzi wake hawakuweza kupata nafasi ya kula chakula. Basi, Yesu akawaambia, “Twendeni peke yetu mahali pa faragha kula chakula, mkapumzike kidogo.”
32 Basi, Wakaondoka peke yao kwa mashua, wakaenda mahali pa faragha.
33 Lakini watu wengi waliwaona wakienda, wakawatambua. Hivyo wengi wakatoka katika kila mji, wakakimbilia huko Yesu na wanafunzi wake walikokuwa wanakwenda, wakawatangulia kufika.
34 Waliposhuka pwani, Yesu aliona umati mkubwa wa watu, akawahurumia, kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji. Akaanza kuwafundisha mambo mengi.
35 Saa za mchana zilikwisha pita. Basi, wanafunzi wakamwendea Yesu, wakamwambia, “Hapa ni nyikani, na sasa kunakuchwa.
36 Afadhali uwaage watu waende mashambani na katika vijiji vya jirani, wanunue chakula.”
37 Lakini Yesu akawaambia, “Wapeni ninyi chakula.” Nao wakamwuliza, “Je, twende kununua mikate kwa fedha dinari mia mbili, na kuwapa chakula?”
38 Yesu akawauliza, “Mnayo mikate mingapi? Nendeni mkatazame.” Walipokwisha tazama, wakamwambia, “Kuna mikate mitano na samaki wawili.”
39 Basi, Yesu akawaamuru wanafunzi wawaketishe watu wote makundimakundi penye nyasi.
40 Nao wakaketi makundimakundi ya watu mia moja na ya watu hamsini.
41 Kisha Yesu akaitwaa ile mikate mitano na wale samaki wawili, akatazama juu mbinguni, akamshukuru Mungu, akaimega mikate, akawapa wanafunzi wake wawagawie watu. Na wale samaki wawili pia akawagawia wote.
42 Watu wote wakala, wakashiba.
43 Wakaokota mabaki ya mikate na samaki pia, wakajaza vikapu kumi na viwili.
44 Nao waliokula hiyo mikate walikuwa wanaume elfu tano.
45 Mara Yesu akawaamuru wanafunzi wake wapande mashua, wamtangulie kwenda Bethsaida, ng'ambo ya ziwa, wakati yeye anauaga umati wa watu.
46 Baada ya kuwaaga watu alikwenda mlimani kusali.
47 Ilipokuwa jioni, mashua ilikuwa katikati ya ziwa, naye alikuwa peke yake katika nchi kavu.
48 Basi, akawaona wanafunzi wake wakitaabika kwa kupiga makasia, maana upepo ulikuwa unawapinga. Karibu na mapambazuko, Yesu aliwaendea akitembea juu ya maji. Alitaka kuwapita.
49 Lakini walimwona akitembea juu ya maji, wakadhani ni mzimu, wakapiga yowe.
50 Maana wote walipomwona waliogopa sana. Mara Yesu akasema nao, “Tulieni, ni mimi. Msiogope!”
51 Kisha akapanda mashuani walimokuwa, na upepo ukatulia. Nao wakashangaa sana.
52 maana hawakuwa bado wameelewa maana ya ile mikate. Akili zao zilikuwa bado zimepumbazika.
53 Walivuka ziwa, wakafika nchi ya Genesareti, wakatia nanga.
Marko 6 in Biblia Takatifu

Marko 6:9-53 in Biblia ya Kiswahili

9 lakini wavae viatu, na siyo kanzu mbili.
10 Na akawaambia, “Nyumba yoyote mtakayoingia, kaeni hapo mpaka mtakapoondoka.
11 Na mji wowote usipowapokea wala kuwasikiliza, ondokeni kwao, kung'uteni mavumbi ya miguu yenu, iwe ushuhuda kwao.”
12 Nao wakaenda wakitangaza watu watubu na kuacha dhambi zao.
13 Waliwafukuza pepo wengi, na waliwapaka mafuta wagonjwa na wakaponywa.
14 Mfalme Herode aliposikia hayo, kwa kuwa jina la Yesu lilikuwa limejulikana sana. Baadhi walisema, “Yohana mbatizaji amefufuka na kwa sababu hiyo, hii nguvu ya miujiza inafanya kazi ndani yake.”
15 Baadhi yao wakasema, “Huyu ni Eliya,” Bado wengine wakasema, “Huyu ni nabii, kama mmoja wa wale manabii wa zamani.”
16 Lakini Herode aliposikia haya akasema, “Yohana, niliyemkata kichwa amefufuliwa.”
17 Maana Herode mwenyewe aliagiza Yohana akamatwe na alimfunga gerezani kwa sababu ya Herodia (mke wa kaka yake Filipo) kwa sababu yeye alikuwa amemuoa.
18 Kwa maana Yohana alimwambia Herode, “Si halali kumuoa mke wa kaka yako.”
19 Lakini Herodia alianza kumchukia na alikuwa akitaka kumuua, lakini hakuweza,
20 maana Herode alimwogopa Yohana; alijua kwamba ni mwenye haki mtu mtakatifu, na alimwacha salama. Na alipoendelea kumsikiliza alihuzunika sana, lakini alifurahi kumsikiliza.
21 Hata ilipofika wakati mwafaka ikiwa imekaribia siku ya kuzaliwa Herode akawaandalia moafisa wake karamu, na makamanda, na viongozi wa Galilaya.
22 Ndipo binti wa Herodia akaingia na kucheza mbele yao, akamfurahisha Herode na wageni walioketi wakati wa chakula cha jioni. Ndipo mfalme akamwambia binti, “Niombe chochote unachotaka nami nitakupa.”
23 Akamwapia na kusema, chochote utakachoniomba, nitakupa, hata nusu ya ufalme wangu.”
24 Akatoka nje akamuuliza mama yake, “Niombe nini?” Akasema, “Kichwa cha Yohana Mbatizaji.”
25 Na mara moja akaingia kwa mfalme akaanza kusema, “Nataka unipatie ndani ya sahani, kichwa cha Yohana Mbatizaji.”
26 Mfalme alisikitishwa sana, lakini kwa sababu ya kiapo chake na kwa ajili ya wageni, hakuweza kumkatalia ombi lake.
27 Hivyo, mfalme akatuma askari kati ya walinzi wake na kuwaagiza kwenda kumletea kichwa cha Yohana. Mlinzi alikwenda kumkata kichwa akiwa kifungoni.
28 Akakileta kichwa chake kwenye sahani na kumpatia binti, na binti akampa mama yake.
29 Na wanafunzi wake waliposikia hayo, walikwenda kuuchukua mwili wake wakaenda kuuzika kaburini.
30 Na mitume, walikusanyika pamoja mbele ya Yesu, wakamweleza yote waliyofanya na waliyoyafundisha.
31 Naye akawaambia, “Njooni wenyewe mahali pa faragha na tupumzike kwa muda.” Watu wengi walikuwa wanakuja na kuondoka, hata hawakupata nafasi ya kula.
32 Hivyo wakapanda mashua wakaenda mahali pa faragha peke yao.
33 Lakini waliwaona wakiondoka na wengi wakawatambua, kwa pamoja walikimbia kwa miguu kutoka miji yote, nao wakafika kabla yao.
34 Walipofika pwani, aliona umati mkubwa na akawahurumia, kwa sababu walikuwa kama kondoo wasiokuwa na mchungaji. Na akaanza kuwafundisha mambo mengi.
35 Muda ulipoendelea sana, wanafunzi wakamjia wakamwambia, “Hapa ni mahali pa faragha na muda umeendelea.
36 Uwaage waende miji ya jirani na vijiji ili wakajinunulie chakula.”
37 Lakini akawajibu akisema, “Wapeni ninyi chakula.” Wakamwambia, “Tunaweza kwenda na kununua mikate yenye thamani ya dinari mia mbili na kuwapa wale?”
38 Akawambia,” Mna mikate mingapi? Nendeni mkaangalie.” walipopata wakamwambia, “Mikate mitano na samaki wawili.”
39 Akawaamuru watu waketi katika makundi juu ya majani mabichi.
40 Wakawaketisha katika makundi; makundi ya mamia kwa hamsini.
41 Kisha akachukua mikate mitano na samaki wawili, na kutazama mbinguni, akaibariki kisha akawapa wanafunzi waweke mbele ya umati. Na kisha aligawa samaki wawili kwa watu wote.
42 Walikula wote hadi wakatosheka.
43 Walikusanya vipande vya mikate iliyobaki, Vikajaa vikapu kumi na viwili, na pia vipande vya samaki.
44 Na walikuwa wanaume elfu tano waliokula mikate.
45 Mara akawaambia wapande kwenye mashua waende sehemu nyingine, hadi Bethsaida, wakati Yeye akiwaaga makutano.
46 Walipokuwa wamekwisha kuondoka, akaenda mlimani kuomba.
47 Kulipokuwa jioni, na mashua yao wakati huo ikiwa katikati ya bahari, naye alikuwa peke yake nchi kavu.
48 Na aliwaona wakitaabika kupiga makasia kwa sababu upepo uliwazuia. Ilipokaribia asubuhi akawaendea, akitembea juu ya maji, na alitaka kuwapita.
49 Lakini walipomwona anatembea juu ya maji, wakaingiwa na wasiwasi wakidhani ni mzimu hata wakapiga kelele.
50 kwa sababu walimwona wakajawa na hofu. Mara akasema nao akawaambia, “Muwe wajasiri! ni mimi! Msiwe na hofu.”
51 Akaingia ndani ya mashua, na upepo ukaacha kuvuma, nao wakamshangaa kabisa.
52 Hivyo hawakuwa wameelewa maana ya ile mikate. Maana akili zao zilikuwa na uelewa mdogo.
53 Nao walipovuka ng'ambo, walifika nchi ya Genesareti mashua ikatia nanga.
Marko 6 in Biblia ya Kiswahili