36 Wakati wakiongea mambo hayo, Yesu mwenyewe alisimama katikati yao, na akawaambia, “Amani iwe kwenu.”
37 Lakini waliogopa na kujawa na hofu, na wakafikiri kwamba waliona roho.
38 Yesu akawaambia, Kwanini mnafadhaika? Kwanini maswali yanainuka mioyoni mwenu?
39 Angalieni mikono yangu na miguu yangu, kwamba ni mimi mwenyewe. Niguseni na muone. Kwa maana roho haina nyama na mifupa, kama mnionavyo mimi kuwa navyo.”
40 Alipokwisha kusema hivi, akawaonyesha mikono yake na miguu yake.
41 Walipokuwa bado na furaha iliyochanganyikana na kutokuamini, na kustaajabu, Yesu akawaambia, “Je mna kitu chochote cha kula?”
42 Wakampa kipande cha samaki aliyechomwa.
43 Yesu akakichukua, na kukila mbele yao.
44 Akawaambia, “Nilipokuwa nanyi, niliwaambia kwamba yote yalioandikwa kwenye sheria ya Musa na manabii na Zaburi lazima yatimilike.”
45 Kisha akafungua akili zao, kwamba waweze kuyaelewa maandiko.
46 Akawaambia, “Kwamba imeandikwa, Kristo lazima ateseke, na kufufuka tena kutoka katika wafu siku ya tatu.
47 Na toba na msamaha wa dhambi lazima ihubiriwe kwa jina lake kwa mataifa yote, kuanzia kutokea Yerusalemu.
48 Ninyi ni mashahidi wa mambo haya.
49 Angalia, nawapelekea ahadi ya Baba yangu juu yenu. Lakini subirini hapa jijini, mpaka mtakapovishwa nguvu kutoka juu.
50 Kisha Yesu akawaongoza nje mpaka walipokaribia Bethania. Akainua mikono yake juu, na akawabariki.
51 Ikatokea kwamba, wakati alipokuwa akiwabariki, aliwaacha na akabebwa juu kuelekea mbinguni.
52 Basi wakamwabudu, na kurudi Yerusalemu na furaha kuu.