Text copied!
Bibles in Swahili (individual language)

Matendo 7:12-51 in Swahili (individual language)

Help us?

Matendo 7:12-51 in Biblia Takatifu

12 Basi, Yakobo alipopata habari kwamba huko Misri kulikuwa na nafaka, aliwatuma watoto wake, yaani babu zetu, waende huko Misri mara ya kwanza.
13 Katika safari yao ya pili, Yosefu alijitambulisha kwa ndugu zake, na Farao akaifahamu jamaa ya Yosefu.
14 Yosefu alituma ujumbe kwa baba yake na jamaa yote, jumla watu sabini na tano, waje Misri.
15 Hivyo, Yakobo alikwenda Misri ambako yeye na babu zetu wengine walikufa.
16 Miili yao ililetwa mpaka Shekemu, ikazikwa katika kaburi Abrahamu alilonunua kutoka kwa kabila la Hamori kwa kiasi fulani cha fedha.
17 “Wakati ulipotimia Mungu aitimize ahadi aliyompa Abrahamu, idadi ya wale watu kule Misri ilikwisha ongezeka na kuwa kubwa zaidi.
18 Mwishowe, mfalme mmoja ambaye hakumtambua Yosefu alianza kutawala huko Misri.
19 Alilifanyia taifa letu ukatili, akawatendea vibaya babu zetu kwa kuwalazimisha waweke nje watoto wao wachanga ili wafe.
20 Mose alizaliwa wakati huo. Alikuwa mtoto mzuri sana. Alilelewa nyumbani kwa muda wa miezi mitatu,
21 na alipotolewa nje, binti wa Farao alimchukua, akamlea kama mtoto wake.
22 Mose alifundishwa mambo yote ya hekima ya Wamisri akawa mashuhuri kwa maneno na matendo.
23 “Alipokuwa na umri wa miaka arobaini aliamua kwenda kuwaona ndugu zake Waisraeli.
24 Huko alimwona mmoja wao akitendewa vibaya, akaenda kumwokoa, na kulipiza kisasi, akamuua yule Mmisri.
25 (Alidhani kwamba Waisraeli wenzake wangeelewa kwamba Mungu angemtumia yeye kuwakomboa, lakini hawakuelewa hivyo.)
26 Kesho yake, aliwaona Waisraeli wawili wakipigana, akajaribu kuwapatanisha, akisema: Ninyi ni ndugu; kwa nini basi, kutendeana vibaya ninyi kwa ninyi?
27 Yule aliyekuwa anampiga mwenzake alimsukuma Mose kando akisema: Ni nani aliyekuweka wewe kuwa kiongozi na mwamuzi wa watu?
28 Je, unataka kuniua kama ulivyomuua yule Mmisri jana?
29 Baada ya kusikia hayo Mose alikimbia, akaenda kukaa katika nchi ya Midiani na huko akapata watoto wawili.
30 “Miaka arobaini ilipotimia, malaika wa Bwana alimtokea Mose katika kichaka kilichokuwa kinawaka moto kule jangwani karibu na mlima Sinai.
31 Mose alistaajabu sana kuona jambo hilo hata akasogea karibu ili achungulie; lakini alisikia sauti ya Bwana:
32 Mimi ni Mungu wa baba zako, Mungu wa Abrahamu, Isaka na Yakobo! Mose akatetemeka kwa hofu na wala hakuthubutu kutazama zaidi.
33 Bwana akamwambia: Vua viatu vyako maana hapa unaposimama ni mahali patakatifu.
34 Nimeyaona mabaya wanayotendewa watu wangu kule Misri. Nimesikia kilio chao, nami nimekuja kuwaokoa. Basi sasa, nitakutuma Misri.
35 “Huyu Mose ndiye yule watu wa Israeli waliyemkataa waliposema: Ni nani aliyekuweka wewe kuwa kiongozi na mwamuzi wetu? Kwa njia ya yule malaika aliyemtokea katika kichaka kilichokuwa kinawaka moto, Mungu alimtuma Mose huyo awe kiongozi na mkombozi.
36 Ndiye aliyewaongoza wale watu watoke Misri kwa kufanya miujiza na maajabu katika nchi ya Misri, katika bahari ya Shamu na jangwani kwa muda wa miaka arobaini.
37 Mose ndiye aliyewaambia watu wa Israeli: Mungu atawateulieni nabii kama mimi kutoka katika ndugu zenu ninyi wenyewe.
38 Wakati watu wa Israeli walipokutana pamoja kule jangwani, Mose ndiye aliyekuwako huko pamoja nao. Alikuwa huko pamoja na babu zetu na yule malaika aliyeongea naye mlimani Sinai; ndiye aliyekabidhiwa yale maneno yaletayo uzima atupe sisi.
39 “Lakini yeye ndiye babu zetu waliyemkataa kumsikiliza; walimsukuma kando, wakatamani kurudi Misri.
40 Walimwambia Aroni: Tutengenezee miungu itakayotuongoza njiani, maana hatujui yaliyompata Mose huyu aliyetuongoza kutoka Misri!
41 Hapo ndipo walipojitengenezea sanamu ya ndama, wakaitambikia na kukifanyia sherehe kitu ambacho ni kazi ya mikono yao wenyewe.
42 Lakini Mungu aliondoka kati yao, akawaacha waabudu nyota za anga, kama ilivyoandikwa katika kitabu cha manabii: Enyi watu wa Israeli! Si mimi mliyenitolea dhabihu na sadaka kwa muda wa miaka arobaini kule jangwani!
43 Ninyi mlikibeba kibanda cha mungu Moloki, na sanamu ya nyota ya mungu wenu Refani. Sanamu mlizozifanya ndizo mlizoabudu. Kwa sababu hiyo nitakupeleka mateka mbali kupita Babuloni!
44 Kule jangwani babu zetu walikuwa na lile hema lililoshuhudia kuweko kwa Mungu. Lilitengenezwa kama Mungu alivyomwambia Mose alifanye; nakala kamili ya kile alichoonyeshwa.
45 Kisha babu zetu walilipokezana wao kwa wao mpaka wakati wa Yoshua, walipoinyakua ile nchi kutoka kwa mataifa ambayo Mungu aliyafukuza mbele yao. Hapo lilikaa mpaka nyakati za Daudi.
46 Daudi alipata upendeleo kwa Mungu, akamwomba Mungu ruhusa ya kumjengea makao yeye aliye Mungu wa Yakobo.
47 Lakini Solomoni ndiye aliyemjengea Mungu nyumba.
48 “Hata hivyo, Mungu Mkuu haishi katika nyumba zilizojengwa na binadamu; kama nabii asemavyo:
49 Bwana asema: Mbingu ni kiti changu cha enzi na dunia ni kiti changu cha kuwekea miguu.
50 Ni nyumba ya namna gani basi mnayoweza kunijengea, na ni mahali gani nitakapopumzika? Vitu hivi vyote ni mimi nimevifanya, au sivyo?
51 “Enyi wakaidi wakuu! Mioyo na masikio yenu ni kama ya watu wa mataifa. Ninyi ni kama baba zenu. Siku zote mnampinga Roho Mtakatifu.
Matendo 7 in Biblia Takatifu

Matendo ya Mitume 7:12-51 in Biblia ya Kiswahili

12 Lakini Yakobo aliposikia kuna nafaka Misri, aliwatuma baba zetu kwa mara ya kwanza.
13 Katika safari ya pili Yusufu akajionyesha kwa ndugu zake, familia ya Yusufu ikajulikana kwa Farao.
14 Yusufu akawatuma ndugu zake kwenda kumwambia Yakobo baba yao aje Misri, pamoja na jamaa yake, jumla ya watu wote ni sabini na tano.
15 Hivyo Yakobo akashuka Misri; kisha akafa yeye pamoja na baba zetu.
16 Wakachukuliwa hata Shekemu wakazikwa katika kaburi ambalo Abrahamu alilinunua kwa vipande vya fedha kutoka kwa wana wa Hamori huko Shekemu.
17 Wakati wa ile ahadi ambayo Mungu alimwahidi Abrahamu ulipokaribia, watu wakiwa wameongezeka huko Misri,
18 wakati huo aliinuka mfalme mwingine juu ya Misri, mfalme asiyejua kuhusu Yusufu.
19 Huyo mfalme mwingine akawadanganya watu wetu na kuwatenda mabaya baba zetu, na kuwatupa watoto wao wachanga ili wasiishi.
20 Katika kipindi kile Musa alizaliwa; alikuwa mzuri mbele za Mungu, akalelewa miezi mitatu katika nyumba ya baba yake.
21 Wakati alipotupwa, binti wa Farao alimchukua akamlea kama mwanaye.
22 Musa alifundishwa mafundisho yote ya Kimisri; alikuwa na nguvu katika maneno na matendo.
23 Lakini baada ya kutimiza miaka arobaini, ikamjia katika moyo wake kuwatembelea ndugu zake, wana wa Israeli.
24 Alipomwona Mwisraeli akitendewa mabaya, Musa alimtetea na kulipiza kisasi aliyekuwa akimwonea kwa kumpiga Mmisiri:
25 akifikiri kuwa ndugu zake watafahamu kwamba Mungu anawaokoa kwa mkono wake, lakini hawakufahamu.
26 Siku iliyofuata akaenda kwa baadhi ya Waisraeli waliokuwa wanagombana; akajaribu kuwapatanisha; akisema,' Mabwana, Ninyi ni ndugu; mbona mnakoseana ninyi kwa ninyi,?
27 Lakini aliyemkosea jirani yake akamsukumia mbali, na kusema, 'Nani kakufanya mtawala na muhukumu wetu?
28 Wewe unataka kuniua, kama ulivyomuua Mmisri jana?”
29 Musa akakimbia baada ya kusikia hivyo; akawa mgeni katika nchi ya Midiani, ambapo akawa baba wa wana wawili.
30 Baada ya miaka arobaini kupita, malaika akamtokea katika jangwa la mlima Sinai, katika mwali wa moto ndani ya kichaka.
31 Wakati Musa alipoona moto, alishangaa na kustaajabia kile alichokiona, na alipojaribu kukisogelea ili kukitazama, sauti ya Bwana ikamjia Ikisema,
32 'Mimi ni Mungu wa baba zako, Mungu wa Abrahamu, na wa Isaka, na wa Yakobo'. Musa alitetemeka na hakuthubutu kuangalia.
33 Bwana akamwambia, 'Vua viatu vyako, sehemu uliposimama ni mahali patakatifu.
34 Nimeona mateso ya watu wangu waliopo Misri; Nimesikia kuugua kwao, nami nimeshuka ili niwaokoe; sasa njoo, nitakutuma wewe Misri.'
35 Huyu Musa ambaye waliyemkataa, wakati waliposema, 'nani kakufanya kuwa mtawala na mwamuzi wetu?'_ alikuwa ndiye ambaye Mungu alimtuma awe mtawala na mkombozi. Mungu alimtuma kwa mkono wa malaika ambaye alimtokea Musa kichakani.
36 Musa aliwaongoza kutoka Misri baada ya kufanya miujiza na ishara katika Misri na katika bahari ya Shamu, na katika jangwa kwa kipindi cha miaka arobaini.
37 Ni Musa huyu ndiye aliyewambia watu wa Isiraeli kuwa, 'Mungu atawainulieni nabii kutoka miongoni mwa ndugu zenu, nabii kama mimi'.
38 Huyu ni mtu ambaye alikuwa katika mkutano jangwani na malaika ambaye aliongea naye katika mlima Sinai. Huyu ndiye mtu ambaye alikuwa na baba zetu, huyu ni mtu ambaye alipokea neno lililo hai na kutupatia sisi.
39 Huyu ni mtu ambaye baba zetu walikataa kumtii; walimsukumia mbali, na katika mioyo yao waligeukia Misri.
40 Katika kipindi hicho walimwambia Haruni. 'tutengenezee miungu itakayotuongoza. Huyo Musa, aliyekuwa akituongoza kutoka katika nchi ya Misri, hatujui kilichompata.'
41 Hivyo wakatengeneza ndama kwa siku hizo na wakatoa sadaka kwa hiyo sananmu na wakafurahi kwa sababu ya kazi ya mikono yao.
42 Lakini Mungu aliwageuza na kuwapa waabudu nyota wa angani, kama ilivyoandikwa kwenye kitabu cha manabii, 'Je Mmenitolea mimi sadaka za wanyama mliowachinja jangwani kwa muda wa miaka arobaini, nyumba ya Israeli?
43 Mmekubali hema ya kukutania ya Moleki na nyota ya mungu refani, na picha mliyoitengeneza na kuwaabudu wao: na nitawapeleka mbali zaidi ya Babeli.'
44 Baba zetu walikuwa na hema ya kukutania ya ushuhuda jangwani, kama Mungu alivyoamuru alipoongea na Musa, kwamba angeitengeneza kwa mfano wa ule aliouona.
45 Hili ni hema ambalo baba zetu, kwa wakati wao, waliletwa katika nchi na Joshua. Hii ilitokea wakati walipoingia kumiliki taifa ambalo Mungu aliwafukuza kabla ya uwepo wa baba zetu. Hii ilikuwa hivi hadi siku za Daudi,
46 ambaye alipata kibali machoni pa Mungu,' na akaomba kutafuta makao kwa Mungu wa Yakobo.
47 Lakini Selemani alimjengea nyumba ya Mungu.
48 Hata hivyo Aliye Juu haishi kwenye nyumba zilizojengwa kwa mikono; hii ni kama nabii alivyosema,
49 Mbingu ni kiti changu cha enzi, na dunia ni sehemu ya kuwekea miguu yangu. Nyumba ya aina gani mtanijengea?, asema Bwana: au ni wapi sehemu yangu ya kupumzikia?
50 Siyo mkono wangu uliofanya hivi vitu vyote?'
51 Enyi watu wenye shingo ngumu msiotahiriwa mioyo na masikio, kila mara mnampinga Roho Mtakatifu,' mnatenda kama baba zenu walivyotenda.
Matendo ya Mitume 7 in Biblia ya Kiswahili