Text copied!
Bibles in Swahili (individual language)

Matendo 16:3-36 in Swahili (individual language)

Help us?

Matendo 16:3-36 in Biblia Takatifu

3 Paulo alitaka Timotheo aandamane naye safarini, kwa hiyo alimtahiri. Alifanya hivyo kwa sababu Wayahudi wote walioishi sehemu hizo walijua kwamba baba yake Timotheo alikuwa Mgiriki.
4 Walipokuwa wanapita katika ile miji waliwapa watu yale maagizo yaliyotolewa na mitume na wazee kule Yerusalemu, wakawaambia wayazingatie.
5 Hivyo, yale makanisa yalizidi kuwa imara katika imani, na idadi ya waumini ikaongezeka kila siku.
6 Walipitia sehemu za Frugia na Galatia kwani Roho Mtakatifu hakuwaruhusu kuhubiri huo ujumbe mkoani Asia.
7 Walipofika kwenye mipaka ya Musia, walijaribu kuingia mkoani Bithunia, lakini Roho wa Yesu hakuwaruhusu.
8 Basi, walipitia Musia, wakaenda moja kwa moja mpaka Troa.
9 Usiku huo, Paulo aliona ono ambalo alimwona mtu mmoja wa Makedonia amesimama pale na kumwomba: “Vuka, uje Makedonia ukatusaidie.”
10 Mara baada ya Paulo kuona ono hilo, tulijitayarisha kwenda Makedonia bila kukawia, tukiwa na hakika kwamba Mungu ametuita tuwapelekee Habari Njema.
11 Kutoka Troa, tulisafiri kwa meli moja kwa moja mpaka Samothrake, na kesho yake tukatia nanga Neapoli.
12 Kutoka huko, tulikwenda mpaka Filipi, mji wa wilaya ya kwanza ya Makedonia, na ambao pia ni koloni la Waroma. Tulikaa katika mji huo siku kadhaa.
13 Siku ya Sabato tulitoka nje ya mji, tukaenda kando ya mto ambapo tulidhani ya kuwa ni mahali pa kusali. Tuliketi, tukaongea na wanawake waliokusanyika mahali hapo.
14 Miongoni mwa wale waliotusikiliza alikuwa mwanamke mmoja mcha Mungu aitwaye Ludia mwenyeji wa Thuatira, ambaye alikuwa mfanyabiashara ya nguo za kitani za rangi ya zambarau. Bwana aliufungua moyo wake hata akayapokea yale maneno Paulo aliyokuwa anasema.
15 Baada ya huyo mama pamoja na jamaa yake kubatizwa, alitualika akisema, “Kama kweli mmeona kwamba mimi namwamini Bwana, karibuni nyumbani kwangu mkakae.” Akatuhimiza twende.
16 Siku moja, tulipokuwa tunakwenda mahali pa kusali, msichana mmoja aliyekuwa na pepo mwenye uwezo wa kuagua alikutana nasi. Msichana huyo alikuwa anawapatia matajiri wake fedha nyingi kwa uaguzi wake.
17 Basi, huyo msichana alimfuata Paulo na sisi, akipiga kelele na kusema, “Hawa watu ni watumishi wa Mungu Mkuu. Wanawatangazieni njia ya wokovu.”
18 Akawa anafanya hivyo kwa siku nyingi hata siku moja Paulo alikasirika, akamgeukia na kumwambia huyo pepo, “Nakuamuru kwa jina la Yesu Kristo, mtoke huyu!” Mara huyo pepo akamtoka.
19 Matajiri wa yule msichana walipoona kwamba tumaini lao la kupata mali limekwisha, waliwakamata Paulo na Sila, wakawaburuta mpaka hadharani, mbele ya wakuu.
20 Wakawashtaki kwa mahakimu wakisema, “Watu hawa ni Wayahudi na wanafanya fujo katika mji wetu.
21 Wanafundisha desturi ambazo sisi raia wa Roma haturuhusiwi kuzikubali wala kuzifuata.”
22 Kundi la watu likajiunga nao, likawashambulia. Wale mahakimu wakawatatulia Paulo na Sila mavazi yao, wakaamuru wapigwe viboko.
23 Baada ya kupigwa sana wakatiwa ndani, na askari wa gereza akaamriwa kuwaweka chini ya ulinzi mkali.
24 Kutokana na maagizo hayo, huyo askari aliwaweka katika chumba cha ndani kabisa cha gereza na kuifunga miguu yao kwenye nguzo.
25 Karibu na usiku wa manane Paulo na Sila walikuwa wakisali na kuimba nyimbo za kumsifu Mungu, huku wafungwa wengine wakiwa wanasikiliza.
26 Ghafla, kulitokea mtetemeko mkuu wa ardhi ambao uliitikisa misingi ya gereza. Mara, milango yote ikafunguka na minyororo iliyowafunga hao wafungwa ikaachana.
27 Askari wa gereza alipoamka na kuiona milango ya gereza imefunguliwa, alidhani kwamba wafungwa wote walikuwa wametoroka na hivyo akauchomoa upanga wake, akataka kujiua.
28 Lakini Paulo akaita kwa sauti kubwa: “Usijidhuru mwenyewe kwa maana sisi sote tuko hapa.”
29 Baada ya kumwita mtu alete taa, huyo askari wa gereza alikimbilia ndani, akajitupa mbele ya miguu ya Paulo na Sila huku akitetemeka kwa hofu.
30 Halafu aliwaongoza nje, akawauliza, “Waheshimiwa, nifanye nini nipate kuokoka?”
31 Wao wakamjibu, “Mwamini Bwana Yesu nawe utaokolewa pamoja na jamaa yako yote.”
32 Basi, wakamhubiria neno la Bwana yeye pamoja na jamaa yake.
33 Yule askari aliwachukua saa ileile ya usiku akawasafisha majeraha yao, kisha yeye na jamaa yake wakabatizwa papo hapo.
34 Halafu akawachukua Paulo na Sila nyumbani kwake, akawapa chakula. Yeye na jamaa yake yote wakafanya sherehe kwa vile sasa walikuwa wanamwamini Mungu.
35 Kesho yake asubuhi, mahakimu waliwatuma maofisa wao wakisema, “Wafungueni wale watu.”
36 Yule askari wa gereza alimpasha habari Paulo: “Mahakimu wametuma ujumbe ili mfunguliwe. Sasa mnaweza kutoka na kwenda zenu kwa amani.”
Matendo 16 in Biblia Takatifu

Matendo ya Mitume 16:3-36 in Biblia ya Kiswahili

3 Paulo alimtaka ili asafiri naye, hivyo akamchukua na kumtahiri kwa sababu ya Wayahudi waliokuwako huko kwani wote walimjua kuwa baba yake ni Mgiriki.
4 Walipokuwa wakienda walipita kwenye miji na kutoa maagizo kwa makanisa ili kuyatii maagizo hayo yaliandikwa na mitume na wazee huko Yerusalemu.
5 Hivyo makanisa yakaimarishwa katika imani na walioamini wakaongezeka kwa idadi kila siku.
6 Paulo na mwenzake wakaenda Firigia na Galatia, kwani Roho wa Mungu aliwakataza kuhubiri neno huko kwenye jimbo la Asia.
7 Walipokaribia Misia, walijaribu kwenda Bithinia, lakini Roho wa Yesu akawakataza.
8 Kwa hiyo wakapita Misia wakaja mpaka Mji wa Troa.
9 Maono yalimtokea Paulo usiku, kulikuwa na mtu wa Makedonia amesimama, akimwita na kusema “Njoni mtusaidie huku Makedonia”.
10 Paulo alipoona maono, mara tukajiandaa kwenda Makedonia, akijua kwamba Mungu alituita kwenda kuwahubiria injili.
11 Hivyo tukaondoka kutoka Troa, tukaenda moja kwa moja Samothrake, na siku iliyofuata tukafika mji wa Neapoli.
12 Kutoka hapo tukaenda Filipi ambao ni moja ya mji wa Makedonia, mji muhimu katika wilaya na utawala wa Kirumi na tukakaa siku kadhaa.
13 Siku ya Sabato, tulikwenda nje ya lango kwa njia ya mto, sehemu ambayo tulidhania kutakuwa na mahali pa kufanyia maombi. Tulikaa chini na kuongea na akinamama waliokuja pamoja.
14 Mwanamke mmoja aitwaye Lidia, muuzaji wa zambarau, kutoka katika mji wa Tiatira, mwenye kumwabudu Mungu, alitusikiliza. Bwana alimfungua moyo wake na kuweka maanani maneno yaliyosemwa na Paulo.
15 Baada ya kubatizwa, yeye na nyumba yake yote, alitusihi akisema “kama mmeniona kuwa mimi ni mwaminifu katika Bwana, basi nawasihi muingie na kukaa kwangu”. Akatusihi sana.
16 Ikawa kwamba, tulipokuwa tunaenda mahali pa kuomba, msichana mmoja aliyekuwa na pepo la utambuzi akakutana nasi. Alimletea bwana wake faida nyingi kwa kubashiri.
17 Mwanamke huyu alimfuata Paulo pamoja na sisi, akipiga kelele na kusema “Hawa wanaume ni watumishi wa Mungu aliye Mkuu, wanaowatangazia ninyi habari ya wokovu”.
18 Alifanya hivyo kwa siku nyingi, lakini Paulo akiwa amekasirishwa na tendo hilo, aligeuka nyuma na kumwambia pepo, “Nakuamuru kwa Jina la Yesu umtoke ndani yake.” Naye akatoka na kumwacha mara moja.
19 Mabwana zake walipoona ya kuwa tumaini la faida yao limeondoka, waliwakamata Paulo na Sila na kuwaburuza sokoni mbele ya wenye mamlaka.
20 Walipowafikisha kwa mahakimu, walisema, “Hawa wanaume ni Wayahudi na wanasababisha ghasia kubwa katika mji wetu.
21 Wanafundisha mambo ambayo siyo sheria sisi kuyapokea wala kuyafuata kama Warumi.”
22 Umati ukawainukia kinyume Paulo na Sila, mahakimu wakararua nguo zao na kuwavua na kuamuru wachapwe viboko
23 Baada ya kuwachapa viboko vingi, waliwatupa gerezani na kumuamuru askari wa gereza kuwalinda vyema.
24 Baada ya kupokea amri hiyo, askari wa gereza aliwatupa katika chumba cha ndani ya gereza na kuwafunga miguu yao kwenye sehemu alipowahifadhi.
25 Wakati wa usiku wa manane, Paulo na Sila wakawa wakiomba na kuimba nyimbo za kumsifu Mungu, huku wafungwa wengine wakiwasikiliza,
26 Ghafla kukatokea tetemeko kuu na misingi ya gereza ikatikiswa, milango ya gereza ikafunguka, na minyororo ya wafungwa wote ikalegezwa.
27 Mlinzi wa Gereza aliamka kutoka usingizini na akaona milango yote ya gereza imefunguliwa; hivyo akachukua upanga wake maana alitaka kujiua kwa sababu alifikiri wafungwa wote walikwishatoroka,
28 Lakini, Paulo akapiga kelele kwa sauti kuu, akisema “usijidhuru kwa sababu wote tuko mahali hapa”.
29 Mlinzi wa gereza aliomba taa ziletwe na akaingia ndani ya gereza kwa haraka, akitetemeka na kuogopa, akawaangukia Paulo na Sila,
30 na kuwatoa nje ya gereza na kusema, “Waheshimiwa, nifanye nini ili nipate kuokoka?”
31 Nao wakamwambia, “Mwamini Bwana Yesu nawe utaokoka pamoja na nyumba yako.”
32 Walinena neno la Bwana kwake, pamoja na watu wote wa nyumbani kwake,
33 Mlinzi wa gereza aliwachukua usiku ule na kuwaosha sehemu walizoumia, yeye pamoja na watu wa nyumbani mwake wakabatizwa mara.
34 Akawaleta Paulo na Sila nyumbani kwake na kuwatengea chakula. Naye akawa na furaha kuu pamoja na watu wa nyumbani mwake kwa sababu walimwamini Mungu.
35 Ilipokuwa mchana, mahakimu walituma ujumbe kwa yule mlinzi wa gereza wakisema, “Waruhusu wale watu waende”,
36 Mlinzi wa gereza akamjulisha Paulo juu ya maneno hayo ya kuwa, “Mahakimu walituma ujumbe niruhusu mwondoke: hivyo tokeni nje na mwende kwa amani.”
Matendo ya Mitume 16 in Biblia ya Kiswahili