Text copied!
Bibles in Swahili (individual language)

Luka 22:12-63 in Swahili (individual language)

Help us?

Luka 22:12-63 in Biblia Takatifu

12 Naye atawaonyesheni chumba kikubwa ghorofani ambacho kimepambwa. Andalieni humo.”
13 Basi, wakaenda, wakakuta kila kitu sawa kama Yesu alivyokuwa amewaambia; wakaandaa karamu ya Pasaka.
14 Saa ilipotimia, Yesu akakaa kula chakula pamoja na mitume wake.
15 Akawaambia, “Nimetamani sana kula Pasaka hii pamoja nanyi kabla ya kuteswa kwangu.
16 Maana nawaambieni, sitaila tena hadi hapo itakapokamilika katika Ufalme wa Mungu.”
17 Kisha akatwaa kikombe, akashukuru akasema, “Pokeeni, mgawanye ninyi kwa ninyi.
18 Kwa maana nawaambieni, sitakunywa tena divai ya zabibu mpaka Ufalme wa Mungu utakapokuja.”
19 Halafu akatwaa mkate, akashukuru, akaumega, akawapa akisema, “Huu ni mwili wangu, unaotolewa kwa ajili yenu. Fanyeni hivi kwa kunikumbuka.”
20 Akafanya vivyo hivyo na kikombe, baada ya chakula, akisema, “Kikombe hiki ni agano jipya linalothibitishwa kwa damu yangu inayomwagika kwa ajili yenu.
21 “Lakini, tazameni! Yule atakayenisaliti yuko nami hapa mezani.
22 Kweli Mwana wa Mtu anakwenda kuuawa kama ilivyopangwa, lakini ole wake mtu anayemsaliti.”
23 Hapo wakaanza kuulizana wao kwa wao ni nani kati yao atakayefanya jambo hilo.
24 Kulitokea ubishi kati ya hao mitume kuhusu nani miongoni mwao anayefikiriwa kuwa mkuu zaidi kuliko wengine.
25 Yesu akawaambia, “Wafalme wa mataifa huwatawala watu wao kwa mabavu, nao huitwa wafadhili wa watu.
26 Lakini isiwe hivyo kati yenu; bali, yule aliye mkuu kati yenu ni lazima awe mdogo wa wote, na aliye kiongozi lazima awe kama mtumishi.
27 Kwa maana, ni nani aliye mkuu: yule anayeketi mezani kula chakula, ama yule anayetumikia? Bila shaka ni yule anayeketi mezani kula chakula! Hata hivyo, mimi niko hapa kati yenu kama mtumishi.
28 “Ninyi ndio mliobaki nami wakati wote wa majaribu yangu;
29 na, kama vile Baba yangu alivyonikabidhi Ufalme, vivyo hivyo nami nitawakabidhi ninyi Ufalme.
30 Mtakula na kunywa mezani pangu katika ufalme wangu, na mtaketi katika viti vya enzi kuyahukumu makabila kumi na mawili ya Israeli.
31 “Simoni, Simoni! Sikiliza! Shetani alitaka kuwapepeta ninyi kama mtu anavyopepeta ngano.
32 Lakini mimi nimekuombea ili imani yako isipungue. Nawe utakaponirudia, watie moyo ndugu zako.”
33 Naye Petro akamjibu, “Bwana, mimi niko tayari kwenda pamoja nawe gerezani, na hata kufa.”
34 Yesu akamjibu, “Nakwambia wewe Petro, kabla jogoo hajawika leo utakuwa umenikana mara tatu.”
35 Kisha, Yesu akawauliza wanafunzi wake, “Wakati nilipowatuma bila mfuko wa fedha wala mkoba wala viatu, mlitindikiwa chochote?” Wakajibu, “La.”
36 Naye akawaambia, “Lakini sasa, yule aliye na mfuko wa fedha auchukue; na aliye na mkoba, hali kadhalika. Na yeyote asiye na upanga, auze koti lake anunue mmoja.
37 Maana nawaambieni, haya maneno ya Maandiko Matakatifu: Aliwekwa kundi moja na wahalifu, ni lazima yatimie. Naam, yale yanayonihusu yanafikia ukamilifu wake.”
38 Nao wakasema, “Bwana, tazama; hapa kuna panga mbili.” Naye akasema, “Basi!”
39 Yesu akatoka, na kama ilivyokuwa desturi yake, akaenda katika mlima wa Mizeituni; wanafunzi wake wakamfuata.
40 Alipofika huko akawaambia, “Salini, msije mkaingia katika kishawishi.”
41 Kisha akawaacha, akaenda umbali wa mtu kuweza kutupa jiwe, akapiga magoti, akasali:
42 “Baba, kama wapenda, ukiondoe kwangu kikombe hiki; hata hivyo, mapenzi yako yatimizwe, wala siyo yangu.”
43 Hapo, malaika kutoka mbinguni, akamtokea ili kumtia moyo.
44 Akiwa katika uchungu mkubwa, alisali kwa bidii zaidi; na jasho likamtoka, kama matone ya damu, likatiririka mpaka chini.
45 Baada ya kusali, aliwarudia wanafunzi wake, akawakuta wamelala, kwani walikuwa na huzuni.
46 Akawaambia, “Mbona mnalala? Amkeni msali, msije mkaingia katika kishawishi.”
47 Alipokuwa bado anaongea, kundi la watu likaja likiongozwa na yule aliyeitwa Yuda, mmoja wa wale mitume kumi na wawili. Yuda akaenda kumsalimu Yesu kwa kumbusu.
48 Lakini Yesu akamwambia, “Yuda! Je, unamsaliti Mwana wa Mtu kwa kumbusu?”
49 Wale wanafunzi wake walipoona hayo wakasema, “Bwana, tutumie panga zetu?”
50 Na mmoja wao akampiga upanga mtumishi wa Kuhani Mkuu, akamkata sikio lake la kulia.
51 Hapo, Yesu akasema, “Acha! Hii inatosha.” Akaligusa sikio la mtu huyo akaliponya.
52 Kisha Yesu akawaambia makuhani wakuu, wakubwa wa walinzi wa Hekalu na wazee waliokuja kumkamata: “Je, mmekuja na mapanga na marungu kunikamata kana kwamba mimi ni mnyang'anyi?
53 Nilipokuwa pamoja nanyi kila siku Hekaluni hamkunitia nguvuni. Lakini, huu ndio wakati wenu hasa, ndio wakati wa utawala wa giza.”
54 Basi, wakamkamata, wakamchukua na kwenda naye nyumbani kwa Kuhani Mkuu. Petro akawa anamfuata nyuma kwa mbali.
55 Moto ulikuwa umewashwa katikati ya ua, nao wakawa wameketi pamoja Petro akiwa miongoni mwao.
56 Mjakazi mmoja alipomwona Petro ameketi karibu na moto, akamkodolea macho, akasema, “Mtu huyu alikuwa pia pamoja na Yesu.”
57 Lakini Petro akakana akisema, “Wee! simjui mimi.”
58 Baadaye kidogo, mtu mwingine akamwona Petro, akasema, “Wewe ni mmoja wao.” Lakini Petro akajibu “Bwana we; si mimi!”
59 Kama saa moja baadaye, mtu mwingine akasisitiza, “Hakika huyu alikuwa pamoja naye; ametoka Galilaya ati.”
60 Lakini Petro akasema, “Bwana wee; sijui hata unachosema!” Na papo hapo, akiwa bado anaongea, jogoo akawika.
61 Bwana akageuka na kumtazama Petro, naye Petro akakumbuka yale aliyokuwa ameambiwa na Bwana: “Leo kabla jogoo hajawika, utanikana mara tatu.”
62 Hapo akatoka nje, akalia sana.
63 Wale watu waliokuwa wanamchunga Yesu, walimpiga na kumdhihaki.
Luka 22 in Biblia Takatifu

Luka 22:12-63 in Biblia ya Kiswahili

12 Atawaonyesha chumba cha ghorofani ambacho kiko tayari. Fanyeni maandalizi humo.”
13 Hivyo wakaenda, na wakakuta kila kitu kama alivyowaambia. Kisha wakaandaa chakula cha Pasaka.
14 Muda ulipofika alikaa na wale mitume.
15 Kisha akawaambia, “Nina shauku kubwa ya kula sikukuu hii ya Pasaka na ninyi kabla ya kuteswa kwangu.
16 Kwa maana nawaambieni, sitakula tena mpaka itakapotimizwa katika ufalme wa Mungu.”
17 Kisha Yesu akachukua kikombe, na alipokwisha kushukuru, akasema, “Chukueni hiki, na mgawane ninyi kwa ninyi.
18 Kwa maana nawaambia, sitakunywa tena mzao wa mzabibu, mpaka ufalme wa Mungu utakapokuja.”
19 Kisha akachukua mkate, na alipokwisha kushukuru, akaumega, na kuwapa, akisema, “Huu ni mwili wangu ambao umetolewa kwa ajili yenu. Fanyeni hivi kwa kunikumbuka mimi.”
20 Akachukua kikombe vivyo hivyo baada ya chakula cha usiku akisema, “Kikombe hiki ni agano jipya katika damu yangu, ambayo imemwagika kwa ajili yenu.
21 Lakini angalieni. Yule anisalitie yuko pamoja nami mezani.
22 Kwa maana Mwana wa Adamu kwa kweli aenda zake kama ilivyokwisha amuliwa. Lakini ole kwa mtu yule ambaye kupitia yeye Mwana wa Adamu asalitiwa!”
23 Wakaanza kuulizana wao kwa wao, nani miongoni mwao ambaye angefanya jambo hili.
24 Kisha yakatokea mabishano katikati yao kwamba ni nani anaye dhaniwa kuwa mkuu kuliko wote.
25 Akawaambia, “Wafalme wa watu wa mataifa wana ubwana juu yao, na wale mwenye mamlaka juu yao wanaitwa waheshimiwa watawala.
26 Lakini haitakiwi kabisa kuwa hivi kwenu ninyi. Badala yake, acha yule ambaye ni mkubwa kati yenu awe kama mdogo. Na yule ambaye ni wa muhimu sana awe kama atumikaye.
27 Kwa sababu yupi mkubwa, yule akaaye mezani au yule anayetumika? Je si yule aketie mezani? Na mimi bado ni kati yenu kama atumikaye.
28 Lakini ninyi ndio ambao mmeendelea kuwa nami katika majaribu yangu.
29 Nawapa ninyi ufalme, kama vile Baba alivyonipa mimi ufalme,
30 kwamba mpate kula na kunywa mezani kwangu kwenye ufalme wangu. Na mtakaa kwenye viti vya enzi mkizihukumu kabila kumi na mbili za Israel.
31 Simoni, Simoni, fahamu kwamba, Shetani ameomba awapate ili awapepete kama ngano.
32 Lakini nimekuombea, kwamba imani yako isishindwe. Baada ya kuwa umerudi tena, waimarishe ndugu zako.”
33 Petro akamwambia, “Bwana, niko tayari kwenda na wewe gerezani na hata katika mauti.”
34 Yesu akajibu, “Nakwambia, Petro, Jogoo hatawika leo, kabla hujanikana mara tatu kwamba unanijua.”
35 Kisha Yesu akawaambia, “Nilipowapeleka ninyi bila mfuko, kikapu cha vyakula, ua viatu, je mlipungukiwa na kitu?” Wakajibu “Hakuna.”
36 Kisha akawaambia, “Lakini sasa, kila mwenye mfuko, na auchukue pamoja na kikapu cha vyakula. Yule ambaye hana upanga imempasa auze joho lake anunue mmoja.
37 Kwa sababu nawaambia, yote ambayo yameandikwa kwa ajili yangu lazima yatimilike, 'Na alichukuliwa kama mtu ambaye anavunja torati.' Kwa sababu kile kilichotabiriwa kwa ajili yangu kinatimizwa.”
38 Kisha wakasema, “Bwana, tazama! Hizi hapa panga mbili.” Na akawaambia “yatosha.”
39 Baada ya chakula cha usiku, Yesu aliondoka, kama ambavyo amekuwa akifanya mara kwa mara, akaenda mlima wa Mzeituni, na wanafunzi wakamfuata.
40 Walipofika, aliwaambia, “Ombeni kwamba msiingie majaribuni.”
41 Akaenda mbali na wao kama mrusho wa jiwe, akapiga magoti akaomba,
42 akisema, “Baba, kama unataka, niondolee kikombe hiki. Lakini si kama nitakavyo mimi, lakini mapenzi yako yafanyike.”
43 Kisha malaika kutoka mbinguni akamtokea, akamtia nguvu.
44 Akiwa katika kuugua, akaomba kwa dhati zaidi, na jasho lake likawa kama matone makubwa ya damu yakidondoka chini.
45 Wakati alipoamka kutoka katika maombi yake, alikuja kwa wanafunzi, na akawakuta wamelala kwa sababu ya huzuni yao,
46 na akawauliza, “Kwanini mnalala? Amkeni muombe, kwamba msiingie majaribuni.”
47 Wakati alipokuwa bado akiongea, tazama, kundi kubwa la watu likatokea, na Yuda, mmoja wa mitume kumi na wawili akiwaongoza. Akaja karibu na Yesu ili ambusu,
48 lakini Yesu akamwambia, “Yuda, je unamsaliti Mwana wa Adamu kwa busu?”
49 Wakati wale waliokuwa karibu na Yesu walipoona hayo yanayotokea, wakasema, “Bwana, je tuwapige kwa upanga?”
50 Kisha mmoja wao akampiga mtumishi wa kuhani mkuu, akamkata sikio lake la kulia.
51 Yesu akasema, “hii inatosha. Na akagusa sikio lake, akamponya.
52 Yesu akasema kwa kuhani mkuu, na kwa wakuu wa hekalu, na kwa wazee waliokuja kinyume chake, “Je mnakuja kana kwamba mnakuja kupambana na mnyang'anyi, na marungu na mapanga?
53 Nilipokuwa pamoja nanyi siku zote kwenye hekalu, hamkuweka mikono yenu juu yangu. Lakini hii ni saa yako, na mamlaka ya giza.”
54 Wakamkamata, wakamuongoza, wakamleta nyumbani mwa kuhani mkuu. Lakini Petro akamfuatilia kwa mbali.
55 Baada ya kuwa wamewasha moto katika ule uwanda wa ndani na walipokwisha kukaa chini pamoja, Petro akakaa katikati yao.
56 Mtumishi mmoja wa kike akamuona Petro alipokuwa amekaa katika mwanga utokanao na moto, akamtazama akamwambia, “Huyu mtu pia alikuwa pamoja naye.”
57 Lakini Petro akakana, akasema, “mwanamke, mimi simjui.”
58 Baada ya muda kidogo, mtu mwingine akamuona akasema “Wewe pia ni mmoja wao”. Lakini Petro akajibu, “Mwanaume, mimi siyo.”
59 Baada ya kama saa moja hivi, mwanaume mmoja akasisitiza akasema, “Kweli kabisa huyu mtu pia alikuwa pamoja naye, maana ni Mgalilaya.”
60 Lakini Petro akasema, “Mwanaume, sijui usemalo.” Na mara, wakati akiongea, jogoo akawika.
61 Akageuka, Bwana akamtazama Petro. Na Petro akalikumbuka neno la Bwana, pale alipomwambia, “Kabla ya jogoo kuwika leo, utanikana mimi mara tatu.”
62 Akienda nje, Petro akalia kwa uchungu mwingi.
63 Kisha wale wanaume waliokuwa wakimlinda Yesu, wakamdhihaki na kumpiga.
Luka 22 in Biblia ya Kiswahili