8 Yesu akajibu, “Muwe waangalifu kwamba msidanganywe. Kwa sababu wengi watakuja kwa jina langu, wakisema, 'Mimi ndiye, 'na 'Muda umekaribia'. Msiwafuate.
9 Mkisikia vita na vuruguvurugu msiogope, kwa sababu haya mambo lazima yatokee kwanza, lakini mwisho hautatokea upesi.”
10 Kisha akawaambia, “Taifa litainuka kupigana na taifa jingine, na ufalme juu ya ufalme mwingine.
11 Kutakuwa na matetemeko makubwa, na njaa na tauni katika maeneo mbalimbali. Kutakuwa na matukio ya kutisha na ishara za kutisha kutoka mbinguni.
12 Lakini kabla ya mambo haya yote, wataweka mikono yao juu yenu na kuwatesa, kuwapeleka kwenye masinagogi na magereza, kuwaleta mbele za wafalme na wenye mamlaka kwa sababu ya jina langu.
13 Hii itawafungulia fursa kwa ushuhuda wenu.
14 Kwahiyo amueni mioyoni mwenu kutoandaa utetezi wenu mapema,
15 kwa sababu nitawapa maneno na hekima, ambayo adui zenu wote hawataweza kuipinga au kuikana.
16 Lakini mtakataliwa pia na wazazi wenu, ndugu zenu, jamaa zenu na rafiki zenu, na watawaua baadhi yenu.
17 Mtachukiwa na kila mmoja kwa sababu ya jina langu.
18 Lakini hakuna hata unywele mmoja wa vichwa vyenu utakaopotea.
19 Katika kuvumilia mtaziponya nafsi zenu.
20 Mtakapoona Yerusalemu imezungukwa na majeshi, basi jueni kwamba uharibifu wake umekaribia.
21 Hapo wale walioko Yudea wakimbilie milimani, na wale walioko katikati ya jiji waondoke, na msiwaache walioko vijijini kuingia.
22 Maana hizi ni siku za kisasi, ili kwamba mambo yote yaliyoandikwa yapate kutimilika.
23 Ole ni kwa wale walio na mimba na kwa wale wanyonyeshao katika siku hizo! Kwa maana kutakuwa na adha kuu juu ya nchi, na ghadhabu kwa watu hawa.
24 Na wataanguka kwa ncha ya upanga na watachukuliwa mateka kwa mataifa yote, na Yerusalem itakanyagwa na watu wa mataifa, mpaka wakati wa watu wa mataifa utakapotimilika.