55 Kama alivyowaahidia wazee wetu Abrahamu na wazawa wake hata milele.”
56 Maria alikaa na Elisabeti kwa muda upatao miezi mitatu, halafu akarudi nyumbani kwake.
57 Wakati wa kujifungua kwake Elisabeti ulifika, akajifungua mtoto wa kiume.
58 Jirani na watu wa jamaa yake walipopata habari kwamba Bwana amemwonea huruma kubwa, walifurahi pamoja naye.
59 Halafu siku ya nane walifika kumtahiri mtoto, wakataka kumpa jina la baba yake, Zakariya.
60 Lakini mama yake akasema, “La, sivyo, bali ataitwa Yohane.”
61 Wakamwambia, “Mbona hakuna yeyote katika ukoo wake mwenye jina hilo?”
62 Basi, wakamwashiria baba yake wapate kujua alitaka mtoto wake apewe jina gani.
63 Naye akaomba kibao cha kuandikia, akaandika hivi: “Yohane ndilo jina lake.” Wote wakastaajabu.
64 Papo hapo midomo na ulimi wake Zakariya vikafunguliwa, akawa anaongea akimsifu Mungu.
65 Hofu ikawaingia jirani wote, na habari hizo zikaenea kila mahali katika milima ya Yudea.
66 Wote waliosikia mambo hayo waliyatafakari mioyoni mwao wakisema: “Mtoto huyu atakuwa mtu wa namna gani?” Maana, hakika nguvu ya Bwana ilikuwa pamoja naye.
67 Zakariya, baba yake mtoto, akajazwa Roho Mtakatifu, akatamka ujumbe wa Mungu:
68 “Asifiwe Bwana Mungu wa Israeli, kwani amekuja kuwasaidia na kuwakomboa watu wake.
69 Ametupatia Mwokozi shujaa, mzawa wa Daudi mtumishi wake.
70 Aliahidi hapo kale kwa njia ya manabii wake watakatifu,
71 kwamba atatuokoa mikononi mwa adui zetu na kutoka mikononi mwa wote wanaotuchukia.
72 Alisema atawahurumia wazee wetu, na kukumbuka agano lake takatifu.
73 Kiapo alichomwapia Abrahamu baba yetu, ni kwamba atatujalia sisi
74 tukombolewe kutoka adui zetu, tupate kumtumikia bila hofu,
75 kwa unyofu na uadilifu mbele yake, siku zote za maisha yetu.