Text copied!
CopyCompare
Biblia ya Kiswahili - Luka - Luka 1

Luka 1:8-42

Help us?
Click on verse(s) to share them!
8Sasa ilitokea kwamba Zakaria alikuwa katika uwepo wa Mungu, akiendelea na wajibu wa kikuhani katika utaratibu wa zamu yake.
9Kulingana na desturi ya kuchagua ni kuhani yupi atakayehudumu, alikuwa amechaguliwa kwa kura kuingia katika hekalu la Bwana na hivyo angefukiza uvumba.
10Kundi lote la watu lilikuwa likiomba nje wakati wa kufukizwa kwa ufumba.
11Sasa malaika wa Bwana alimtokea na kasimama upande wa kulia wa madhabahu ya kufukizia.
12Zakaria alitishika alipomuona; hofu ikamwangukia.
13Lakini malaika akamwambia, “Usiogope Zakaria, kwasababu maombi yako yamesikika. Mke wako Elizabeth atakuzalia mwana. Jina lake utamwita Yohana.
14Utakuwa na furaha na uchangamfu, na wengi watakufurahia kuzaliwa kwake.
15Kwa kuwa atakuwa mkuu mbele ya macho ya Bwana. Hatakunywa divai au kinywaji kikali, na atakuwa amejazwa na Roho Mtakatifu tangu tumboni mwa mama yake.
16Na watu wengi wa Israel watageuzwa kwa Bwana Mungu wao.
17Atakwenda mbele za uso wa Bwana katika roho na nguvu ya Eliya. Atafanya hivi ili kurejesha mioyo ya baba kwa watoto, ili kwamba wasiotii wataenenda katika hekima ya wenye haki. Atafanya hivi kuweka tayari kwa Bwana watu ambao wameandaliwa kwa ajili yake.”
18Zakaria akamwambia malaika, “Nitawezaje kujua hili? Kwasababu mimi ni mzee na mke wangu miaka yake imekuwa mingi sana.”
19Malaika akajibu na kumwambia, “Mimi ni Gabrieli, ambaye husimama mbele za Mungu. Nilitumwa kukwambia, kukuletea habari hii njema.
20Na tazama, hutaongea, utakuwa kimya, hutaweza kuongea mpaka siku ile mambo haya yatakapotokea. Hii ni kwasababu ulishindwa kuamini maneno yangu ambayo yatatimizwa kwa wakati mwafaka.”
21Sasa watu walikuwa wakimsubiri Zakaria. Walishangazwa kwamba alikuwa anatumia muda mwingi hekaluni.
22Lakini alipotoka nje, hakuweza kuongea nao. Wakatambua kwamba alikuwa amepata maono alipokuwa hekaluni. Aliendelea kuonesha ishara na alibaki kimya.
23Ikatokea kwamba siku za huduma yake zilipokwisha aliondoka kurudi nyumbani kwake.
24Baada ya Zakaria kurudi nyumbani kutoka kwenye huduma yake hekaluni, mke wake akawa mjamzito. Naye hakutoka nyumbani mwake kwa muda wa miezi mitano. Akasema,
25“Hili ndilo amabalo Bwana amefanya kwangu aliponitazama kwa upendeleo ili kuiondoa aibu yangu mbele za watu.”
26Sasa, katika mwezi wa sita wa mimba ya Elizabeti, Mungu alimwambia malaika Gabrieli kwenda kwenye mji wa Galilaya uitwao Nazareti,
27kwa bikra aliyekuwa ameposwa na mwanaume ambaye jina lake lilikuwa Yusufu. Yeye alikuwa wa ukoo wa Daudi, na jina la bikra huyo lilikuwa Mariamu.
28Akaja kwake na akasema, “Salaam, wewe uliyepokea neema kuu! Bwana amependezwa nawe.”
29Lakini maneno ya malaika yalimchanganya na hakuelewa kwa nini malaika alisema salaam hii ya ajabu kwake.
30Malaika akamwambia, “Usiogope, Mariamu, maana umepata neema kutoka kwa Mungu.
31Na tazama, utabeba mimba katika tumbo lako na utazaa mwana. Nawe utamwita jina lake 'Yesu.'
32Atakuwa mkuu na ataitwa Mwana wa Aliye Juu Sana. Bwana Mungu atampa kiti cha enzi cha Daudi baba yake.
33Atatawala juu ya ukoo wa Yakobo milele na ufalme wake hautakuwa na mwisho.
34Mariamu akamwambia malaika, hili litatokea kwa namna gani, maana sijawahi kulala na mwanaume yeyote?
35Malaika akajibu na akamwambia, “Roho Mtakatifu atakujia juu yako, na nguvu ya Aliye Juu Sana itakuja juu yako. Kwa hiyo, mtakatifu atakayezaliwa ataitwa Mwana wa Mungu.
36Na tazama, ndugu yako Elizabeti anaujauzito wa mwana kwenye umri wake wa uzee. Huu ni mwezi wa sita kwake, ambaye alikuwa anaitwa mgumba.
37Maana hakuna lisilowezekana kwa Mungu.”
38Mariamu akasema, “Tazama, mimi ni mtumishi wa kike wa Bwana. Acha iwe hivyo kwangu sawa sawa na ujumbe wako.” Kisha malaika akamwacha.
39Ndipo katika siku hizo Mariamu aliondoka na kwa haraka alikwenda katika nchi ya vilima, kwenye mji katika nchi ya Yudea.
40Alikwenda nyumbani mwa Zekaria na akamsalimia Elizabeti.
41Sasa, ilitokea kwamba Elizabeti aliposikia salamu ya Mariamu, mtoto tumboni mwake akaruka, na Elizabeti akajazwa na Roho Mtakatifu.
42Akapaza sauti yake na kusema kwa sauti kuu, “umebarikiwa wewe zaidi miongoni mwa wanawake, na mtoto aliyemo tumboni mwako amebarikiwa.

Read Luka 1Luka 1
Compare Luka 1:8-42Luka 1:8-42