Text copied!
CopyCompare
Biblia ya Kiswahili - Marko

Marko 14

Help us?
Click on verse(s) to share them!
1Ilikuwa siku mbili tu baada ya sikukuu ya Pasaka na ya Mikate Isiyotiwa Chachu. Makuhani wakuu na waandishi walikuwa wakitafuta namna ya kumkamata Yesu kwa hila na kumuua.
2Kwa kuwa walisema, “Sio wakati huu wa sikukuu, watu wasije wakafanya ghasia.”
3Wakati Yesu alipokuwa Bethania nyumbani kwa Simoni mkoma, na alipokuwa akielekea mezani, mwanamke mmoja alikuja kwake akiwa na chupa ya marashi ya nardo safi yenye gharama kubwa sana, aliivunja chupa na kuimimina juu ya kichwa chake.
4Lakini kulikuwa na baadhi yao waliokasirika. Waliambiana wao kwa wao wakisema, “Ni nini sababu ya upotevu huu?
5Manukato haya yangeweza kuuzwa kwa zaidi ya dinari mia tatu, na wakapewa maskini.” Nao walimkemea.
6Lakini Yesu alisema, “Mwacheni peke yake. Kwa nini mnamsumbua? Amefanya jambo zuri kwangu.
7Siku zote maskini mnao, na wakati wowote mnapotamani mnaweza kufanya mazuri kwao, lakini hamtakuwa nami wakati wote.
8Amefanya kile anachoweza: ameupaka mwili wangu mafuta kwa ajili ya maziko.
9Kweli nawaambia, kila mahali injili inapohubiriwa katika ulimwengu wote, kile alichofanya mwanamke huyu kitazungumzwa kwa ukumbusho wake.
10Kisha Yuda Iskariote, mmoja wa wale kumi na wawili, alikwenda kwa wakuu wa makuhani ili kwamba apate kumkabidhi kwao.
11Wakati wakuu wa Makuhani waliposikia hivyo, walifurahi na wakaahidi kumpa fedha. Alianza kutafuta nafasi ya kumkabidhi kwao.
12Katika siku ya kwanza ya mkate usiotiwa chachu, wakati walipotoa mwanakondoo wa pasaka, wanafunzi wake walimwambia, “Unataka twende wapi tukaandae ili upate kula mlo wa Pasaka?”
13Aliwatuma wanafuzi wake wawili na kuwaambia, “Nendeni mjini, na mwanamume ambaye amebeba mtungi ataonana nanyi. Mfuateni.
14Nyumba atakayoingia, mfuateni na mmwambie mwenye nyumba hiyo, 'Mwalimu asema, “Kiko wapi chumba cha wageni mahali nitakapokula Pasaka na wanafunzi wangu?”
15Atawaonesha chumba cha juu kikubwa chenye samani ambacho kiko tayari. Fanyeni maandalizi kwa ajili yetu pale.”
16Wanafunzi waliondoka wakaenda mjini; walikuta kila kitu kama alivyokuwa amewaambia, na wakaandaa mlo wa Pasaka.
17Wakati ilipokuwa jioni, alikuja na wale Kumi na wawili.
18Na walipokuwa wakiikaribia meza na kula, Yesu alisema, “Kweli nawaambia, mmoja kati yenu anayekula pamoja nami atanisaliti.”
19Wote walisikitika, na mmoja baada ya mwingine walimwambia, “Hakika siyo mimi?”
20Yesu alijibu na kuwaambia, “Ni mmoja wa Kumi na wawili kati yenu, mmoja ambaye sasa anachovya tonge katika bakuli pamoja nami.
21Kwa kuwa Mwana wa Adamu atakwenda kama vile maandiko yasemavyo juu yake. Lakini ole wake mtu yule ambaye kupitia yeye Mwana wa Adamu atasalitiwa! Ingekuwa vizuri zaidi kwake kama mtu yule asingezaliwa.”
22Na walipokuwa wakila, Yesu alichukua mkate, akaubariki, na kuumega. Aliwapa akisema, “Chukueni. Huu ni mwili wangu.”
23Alichukua kikombe, akashukuru, na akawapatia, na wote wakakinywea.
24Aliwaambia, “Hii ni damu yangu ya agano, damu imwagikayo kwa ajili ya wengi.
25Kweli nawaambia, sitakunywa tena katika zao hili la mzabibu mpaka siku ile nitakapokunywa mpya katika ufalme wa Mungu.”
26Walipokwisha kuimba wimbo, walikwenda nje katika Mlima wa Mizeituni.
27Yesu aliwaaambia, “Ninyi nyote mtajitenga mbali kwa sababu yangu, kwa kuwa imeandikwa, 'Nitampiga mchungaji na kondoo watatawanyika.'
28Lakini baada ya kufufuka kwangu, nitawatangulia mbele yenu Galilaya.”
29Petro alimwambia, “Hata kama wote watakuacha, mimi sitakuacha.”
30Yesu alimwambia, “Kweli nakuambia, usiku huu, kabla jogoo hajawika mara mbili, utakuwa umenikana mara tatu.”
31Lakini Petro alisema, “Hata itanilazimu kufa pamoja nawe, sitakukana.” Wote walitoa ahadi ile ile.
32Walikuja kwenye eneo lililoitwa Gethsemane, na Yesu akawaambia wanafunzi wake, “Kaeni hapa wakati nasali.”
33Aliwachukua Petro, Yakobo, na Yohana pamoja naye, akaanza kuhuzunika na kutaabika sana.
34Aliwaambia, “Nafsi yangu ina huzuni sana, hata kufa. Bakini hapa na mkeshe.”
35Yesu alienda mbele kidogo, akaanguka chini, akaomba, kama ingewezekana, kwamba saa hii ingemwepuka.
36Alisema, “Aba, Baba, Mambo yote kwako yanawezekana. Niondolee kikombe hiki. Lakini siyo kwa mapenzi yangu, bali mapenzi yako.”
37Alirudi na kuwakuta wamelala, na akamwambia Petro, “Simoni, je umelala? Hukuweza kukesha hata saa moja?
38Kesheni na muombe kwamba msije mkaingia katika majaribu. Hakika roho i radhi, lakini mwili ni dhaifu.”
39Alienda tena na kuomba, na alitumia maneno yaleyale.
40Alikuja tena akawakuta wamelala, kwa kuwa macho yao yalikuwa mazito na hawakujua nini cha kumwambia.
41Alikuja mara ya tatu na kuwaambia, “Bado mmelala na kupumzika? Yatosha! Saa imefika. Tazama! Mwana wa Adamu atasalitiwa mikononi mwa wenye dhambi.
42Amkeni, twendeni. Tazama, yule anayenisaliti yuko karibu.”
43Mara tu alipokuwa bado anaongea, Yuda, mmoja wa wale kumi na wawili, alifika, na kundi kubwa kutoka kwa wakuu wa makuhani, waandishi na wazee wenye mapanga na marungu.
44Wakati huo msaliti wake alikuwa amewapa ishara, akisema, Yule nitakayembusu, ndiye. Mkamateni na kumpeleka chini ya ulinzi.”
45Wakati Yuda alipofika, moja kwa moja alienda kwa Yesu na kusema, “Mwalimu!” Na akambusu.
46Kisha wakumtia chini ya ulinzi na kumkamata.
47Lakini mmoja kati yao aliyesimama karibu naye alichomoa upanga wake akampiga mtumishi wa kuhani mkuu na kumkata sikio.
48Yesu aliwaambia, “Mmekuja kunikamata kwa mapanga na marungu kama mnyang'anyi?
49Wakati kila siku nilikuwa nanyi na nikifundisha hekaluni, hamkunikamata. Lakini hili limefanyika ili maandiko yatimie.
50Na wale wote waliokuwa na Yesu walimwacha na kukimbia.
51Kijana mmoja alimfuata, aliyekuwa amevaa shuka tu aliyokuwa amejifunika kumzunguka; walimkamata lakini
52aliwaponyoka akaiacha shuka pale akakimbia uchi.
53Walimwongoza Yesu kwa kuhani mkuu. Pale walikusanyika pamoja naye makuhani wakuu wote, wazee, na waandishi.
54Petro naye alimfuata Yesu kwa mbali, kuelekea kwenye ua wa kuhani mkuu. Aliketi pamoja na walinzi, waliokuwa karibu na moto wakiota ili kupata joto.
55Wakati huo makuhani wakuu wote na Baraza lote walikuwa wakitafuta ushahidi dhidi ya Yesu ili wapate kumwua. Lakini hawakuupata.
56Kwa kuwa watu wengi walileta ushuhuda wa uongo dhidi yake, lakini hata ushahidi wao haukufanana.
57Baadhi walisimama na kuleta ushahidi wa uongo dhidi yake; wakisema,
58“Tulimsikia akisema, 'Nitaliharibu hekalu hili lililotengenezwa kwa mikono, na ndani siku tatu nitajenga lingine lisilotengenezwa kwa mikono.'”
59Lakini hata ushahidi wao haukufanana.
60Kuhani mkuu alisimama katikati yao na akamwuliza Yesu, “Je, huna jibu? Watu hawa wanashuhudia nini dhidi yako?”
61Lakini alikaa kimya na hakujibu chochote. Mara Kuhani mkuu alimwuliza tena, “Je wewe ni Kristo, mwana wa Mbarikiwa?”
62Yesu alisema, “Mimi ndiye. Na utamwona Mwana wa Adamu ameketi mkono wa kulia wa nguvu akija na mawingu ya mbinguni.”
63Kuhani mkuu alirarua mavazi yake na kusema, “Je, bado tunahitaji mashahidi?
64Mmesikia kufuru. Uamuzi wenu ni upi?” Na wote walimhukumu kama mmoja aliyestahili kifo.
65Baadhi wakaanza kumtemea mate na kumfunika uso na kumpiga na kumwambia, “Tabiri!” Maafisa walimchukua na kumpiga.
66Na Petro alipokuwa bado yuko chini uani, mtumishi mmoja wa wasichana wa kuhani mkuu alikuja kwake.
67Alimwona Petro alipokuwa amesimama akiota moto, na alimtazama kwa kumkaribia. Kisha alisema, “Nawe pia ulikuwa na Mnazareti, Yesu”.
68Lakini alikataa, akisema, “Sijui wala sielewi kuhusu kile unachosema!” Kisha alitoka akaenda nje uani. (Zingatia; Mstari huu, “Na jogoo akawika” haumo kwenye nakala za kale).
69Lakini mtumishi wa kike pale, alimwona na alianza kuwaambia tena wale ambao walikuwa wamesimama pale, “Mtu huyu ni mmoja wao!”
70Lakini alikana tena. Baadaye kidogo wale waliokuwa wamesimama pale walikuwa wakimwambia Petro, “Hakika wewe ni mmoja wao, kwa maana wewe pia ni Mgalilaya.”
71Lakini alianza kujiweka mwenyewe chini ya laana na kuapa, “Simjui mtu huyu mnayemsema.”
72Kisha jogoo aliwika mara ya pili. Kisha Petro alikumbuka maneno ambayo Yesu aliyokuwa amemwambia: “Kabla jogoo hajawika mara mbili, utanikana mara tatu.” Na alianguka chini na kulia.